Monday 5 March 2018

Kim Jong-un akutana na ujumbe kutoka Korea Kusini


Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-un anaandaa mkutano wa chakula cha jioni na wajumbe wawili kutoka Korea Kusini, ikiwa ndiyo mara ya kwanza kiongozi huyo anakutana na ujumbe kutoka Kusini tangu aingie madarakani mwaka 2011.

Shirika la habari la Korea Kusini la Yonhap, liliripoti kuhusu mkutano huo likimnukuu msemaji wa rais nchini Korea Kusini.

Ujumbe huo uko nchini Korea Kaskazini kwa mazungumzo yasiyo ya kawaida yenye lenngo la kuanzisha mchakato kati ya Korea Kaskazini na Marekani.

Uhusiano kati ya nchi hizo mbili umeboreka kufuata mashindano ya olimpiki ya msimu wa baridi.

Ujumbe huo unawajumuisha maafisa wenye vyeo vya mawaziri - mkuu wa ujasusi Suh Hoon na mshauri wa usalama wa taifa Chung Eui-yong.

Awali Bw Chung aliwaambia waandishi wa habari kuwa atawasilisha azimio la Rais Moon Jae-in la kudumisha mazungumzo na kuboresha uhusiano kati ya Korea Kaskazini na Kusini na kuondoa silaha za nyuklia kutoka Rasi wa Korea.

Rais wa Marekani Donald Trump alisema Jumapili kuwa Marekani itakuwa tayari kukutana na Korea Kaskazini lakini akasisitiza kuwa Korea ni lazima iondoe zana zake za nyuklia.

Hata hivyo Korea Kaskazini ambayo imesema inataka kufanya mazungumzo na Marekani, imesema kuwa ni hatua ya "kishenzi" kuwa Marekani inataka kuwepo masharti.

Haijulikani ni nani atawakilisha Marekani ikiwa mkutano kama huo utafanyika.

Mjumbe mkuu wa Marekani kuhusu Korea Kaskazini Joseph Yun alitangaza uamuzi wake wa kustaafu mapema wiki iliyopita.

Wadadisi wanaamini kuwa Bw Yun alikuwa akipendelea sana suluhu ya kidiplomasia na Korea Kaskazini.

0 comments:

Post a Comment