Wednesday, 20 December 2017

Sugu awashangaa wanachama wa CCM


Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema),  Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ amewashangaa wananchama wa CCM waliolipigia hesabu jimbo hilo, akidai kuwa wanajisumbua kwa sababu walishapoteana tangu mwaka 2010.

Akizungumza leo Desemba 20 katika mahojiano maalum na MCL Digital, Sugu amesema viongozi wa CCM wanaojipambanua kutaka chama hicho kishinde majimbo ya upinzani, ikiwa ni pamoja na kuongoza halmashauri wanapoteza muda.

“Wanataka kurudisha jiji la Mbeya mikononi mwao sambamba na kata zote ambazo tulishinda katika uchaguzi uliopita. Wanajisumbua,” amesema.

Sugu alikuwa akimjibu Mwenyekiti mpya wa CCM mkoani Mbeya,  Jacob Mwakasole ambaye mara baada ya ushindi huo ameshangazwa na upinzani mkali uliopo katika jiji hilo.

Mwakasole amesema  mkoa huo unazo changamoto nyingi za kisiasa na makundi ndani ya CCM, kuwataka wanachama  kushikamana kuzishughulikia ili kurudisha nguvu ya chama hicho ili kulirejesha jimbo hilo mikononi mwa CCM.

 “Ni wazi CCM wamepaniki na kuparanganyika tangu mwaka 2010. Wanapaswa kutambua kuwa sisi pia hatujalala na ushindi wetu wa mwaka 2015 umetokana na wananchi kuridhia na uchapaji kazi wa Chadema,” amesema.

Amesema Chadema bado kina nguvu kubwa, Uchaguzi Mkuu ujao kitashinda kwa kishindo katika jimbo hilo, nchi nzima.

0 comments:

Post a Comment